settings icon
share icon
Swali

Je, kweli Biblia inafundisha kuwa na mke mmoja?

Jibu


Ndoa ya mke mmoja ni tabia au hali ya kuoleka na mtu mmoja tu kwa wakati mmoja. Mungu alipoanzisha agano la ndoa, Alipanga uhusiano kuwa wa mke mmoja. Katika Mwanzo 2:21-22, Mungu alimuumba Adamu na kisha akamuumba mwanamke, Hawa, kutoka kwenye ubavu wake mmoja na kumleta kwa mwanamume. Mungu hakumuumbia Adamu wanawake kadhaa, jambo amblo lingesaidia katika kutimiza amri ya kuijaza dunia (Mwanzo 1:27-28). Adamu alijibu kwa tangazo la shangwe kwamba Hawa alikuwa “mfupa wa mfupa wangu na nyama ya nyama yangu” (mstari wa 23), ikifuatwa na tangazo hili: “Kwa sababu hii mwanaume atamwacha baba yake na mama yake na kuambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja” (mstari 24). Yesu aliunga mkono ukweli huu alipoulizwa kuhusu talaka (Mathayo 19:5). Kisha akaongeza, “Hivyo si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe” (Mathayo 19:6). Tangu mwanzo kabisa wa Biblia, ndoa ya mke mmoja ndicho kielelezo.

Agano la Kale lina mifano mingi ya watu waliotelekeza desturi ya ndoa ya mke mmoja. Wazee na wafalme wengi walikuwa na wake wengi. Hata Daudi na Sulemani, viongozi waliochaguliwa na Mungu, walizidisha wake katika kipindi cha utawala wao, na Biblia haisemi juu ya uvunjaji huu dhaihiri wa utauwa. Kumbukumbu la Torati 17:17 inawakataza wafalme wa Israeli haswa dhidi ya kuoa wake wengi. Na kwa sababu Biblia ni aminifu sana kuhusu ubinidadmu na kushindwa kwa hata wale ambao Mungu aliwatumia kwa nguvu nyingi, inaandika kwa uwajibikaji matatizo ambayo wake walioongezeka waliumba.

Katika kila simulizi ya Biblia ya wanaume kuwa na wake wegni, kuna migogoro. Familia zisizo na msingi wa uhusiano wa mke mmoja zililipa gharama. Ibrahimu, Sarai, na Hagari walikuwa “mzunguko wa upeno” ulioharibika—wivu ulitokea wakati Hagari alipopata mimba wakata Sarai ambaye alikuwa mke mkubwa hangeweza kupata mimba (Mwanzo 16:1-5). Raheli na Lea walishdinana kwa ajili ya mapenzi ya Yakobo, ambayo yalisababisha kuleta vijakazi kuwa Masuria wa mume wao (Mwanzo 30). Nabii Samweli alizaliwa katika nyumba ambayo mama yake Hana alikasirishwa kila mara na mke mwenza, Penina (1 Samweli 1:4-6).

Katika nyumba ya Mfalme Daudi, kuongezeka kwa wake na watoto kuliongeza hali ya kutofanya kazi vizuri hivi kwamba wangeweza kuwa kipindi cha uhalisia wao wenyewe. Tamari bintiye Daudi kutoka kwa mke mmoja alinajisiwa na mwanawe Amnoni kutoka kwa mke mwingine (2 Samweli 13). Absalomu, ndugu ya Tamari, alipopata habari za fedheha yake, alipanga njama ya kulipiza kisasi kisha akamuua Amnoni, nduguye wa kambo. Huenda Daudi kukosa kushughulikia tatizo katika familia yake kulimfanya mwanawe Absalom kumchukia na kujaribu kutwaa kiti cha ufalme. Kama Daudi angekubali kuwa na mke mmoja, hakuna uchungu huu wa moyo ungetokea, na huenda hangelazimika kukimbia kuokoa maisha yake kutoka kwa mwanawe mwenyewe (2 Samweli 15:14).

Hadithi ya Sulemani, haswa, inaonyesha upumbavu wa kuchukua wake wengi. Mfalme Sulemani alikuwa amepewa kila kitu ambacho moyo wake ulitamani. Mungu alikuwa amempa hekima zaidi ya wanadamu wengi (1 Wafalme 4:29-30) na alikuwa amembariki kimwili pia (1 Wafalme 10:23). Mungu alikuwa amempa “utulivu kila upande hakuna adui wala maafa” (1 Wafalme 5:4). Sulemani alipewa heshima kubwa ya kujenga hekalu la Bwana (1 Wafalme 5:5). Hata hivyo alikuwa ameoa wake wengi kutoka nchi nyingi, na, katika uzee wake, moyo wake ulimwacha Bwana kwa sababu ya ibada ya sanamu ya wake zake (1 Wafalme 11:3-4). Ikiwa sulemani angejitosheka na mke mmoja, hangekumbana na jaribu kama hilo na angebaki mwaminifu kwa Bwana hadi kufa kwake.

Kufikia nyakati za Agano Jipya, ndoa ya mke mmoja ilikuwa ni kawaida katika utamaduni wa Kiyahudi. Yesu alifundisha ndoa ya mke mmoja. Yesu alipoulizwa kuhusu talaka, jibu Lake lilidokeza kwa uthabiti kwamba ndoa ni kati ya mwanamume mmoja na mwanamke mmoja, bila dokezo lolote la mitala: “Lakini tangu mwanzo wa uumbaji, ‘Mungu aliwaumba mwanaume na mwanamke. Kwa sababu hii mwanaume atamwacha baba yake na mama yake na kuambatana na mkewe, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.’ Kwa hiyo hawatakuwa wawili tena, bali mwili mmoja. Basi, alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe” (Marko 10:6-9). Yesu anaposema kwamba “wawili hao watakuwa mwili mmoja,” maana iliyo wazi ni kwamba muungano huo ni kati ya watu wawili pekee. Sio watatu au zaidi wanakuwa mwili mmoja; wawili tu wanakuwa mmoja. Hakuna mahli ambapo Yesu au mwandishi yeyote wa Agano Jipya anapendekeza muungano huu ufanyike kati ya mtu aliyeolewa na mtu mwingine.

Kwa hakika, wakati Paulo anatoa amri za wazi kuhusu ndoa, anarejelea kifungu kuhusu kuwa “mwili mmoja” na kulinganisha na Kristo na bibi-arusi Wake, kanisa (Waefeso 5:32). Anamalizia kwa kumuagiza mume ampende mke wake kama anavyojipenda mwenyewe (mstari 33). Hamwambii mume “wapende wake zako wote.” Neno mke liko katika hali ya umoja. Ni kupita mipaka kujaribu kutekeleza amri ya kuwa “mwili mmoja” kwa mwanamume na wanawake kadhaa. Na biblia haidokezi kamwe kwamba ndoa inaweza kuunganisha chochote isipokuwa mwanamume na mwanamke. Dhana ya ndoa ya watu wa jinsia moja ni mkanganyiko wa maneno.

Maandiko hayazungumzii moja kwa moja desturi ya mitala katika Agano la Kale, lakini nia ya awali ya Mungu ya ndoa ilikuwa wazi kuwa mke mmoja. Biblia inaonyesha matokeo ya kuwa na wake wengi, na haisemi kuwa na wake wengi kwa njia nzuri. Ndoa inapaswa kuwa picha ya agano ambalo Kristo analo na kanisa lake (2 Wakorintho 11:2), picha inayolingana vizuri na mpango wa Mungu kwamba ndoa ni ya mwanamume mmoja na mwanamke mmoja katika maisha yote.

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je, kweli Biblia inafundisha kuwa na mke mmoja?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries