settings icon
share icon
Swali

Je, imani inaweza kubadilisha mpango wa Mungu?

Jibu


Jibu fupi ni kwamba hakuna kitu kinachoweza kubadilisha mpango kamili wa Mungu. Hata hivyo, Mungu anaweza kutoa na huwa anatoa karama ya imani na kufanya kazi kupitia imani hiyo ndani ya mtu ili kutimiza mpango Wake. Kwa hivyo, kwa mtazamo wetu wa kibinadamu, mara nyingi inaonekana kwamba matumizi yetu ya imani hubadilisha jinsi Mungu anavyofanya kazi.

Kwa mfano, nyakati zingine Yesu aliwaponya watu na kusema, “Imani yako imekuponya” (Mathayo 9:22; Luka 17:19). Katika Marko 6:1-6 na Mathayo 13:53-58, Yesu akifundisha katika Nazareth mji wake wa nyumbani, na wenyeji walimkataa. Marko anasema, “Hakufanya miujiza yoyote huko isipokuwa kuweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache na kuwaponya. Naye akashangazwa sana kwa jinsi wasivyokuwa na imani” (Marko 6:5-6). Kwa hivyo, Biblia ina mifano ya Mungu akitenda (au kutotenda) katika jibu la moja kwa moja kwa imani ya watu (au ukosefu wake). Je, imani ya mtu binafsi inabadilisha mpango wa Mungu? Kwa mtazamo wa kibinadamu, inaonekana Yesu, Mungu Mwana, alifanya jambo tofauti kulingana na kiwango cha imani katika mtu mwingine. Hata hivyo, kwa mtazamo wa Mungu, tayari alijua ni nani ambaye angemponya na ambaye hatamponya. Kwa maana hiyo, mpango wa Mungu haukubadilishwa.

Ugumu wa swali la ikiwa imani inabadilisha mpango wa Mungu unagusa swali kubwa la mapenzi ya Mungu na uamuzi wa mwanadamu. Mungu anayajua mambo yote, na ana mpango kamilifu. Hata hivyo, Yeye pia anaamuru watu kufanya mambo fulani, huku akikamilisha mpango Wake kupitia wanadamu. Pia, Mungu aliruhusu dhambi kuingia ulimwenguni na anaruhusu mateso bado hii leo. Mambo haya si sehemu ya mapenzi ya Mungu, lakini ni sehemu ya mapenzi Yake yanayoruhusu. Mpango kuu wa Mungu kwa wanadamu, na njia Anapaswa kuchukua ndio huo mpango utimie, ni kubwa mno na ngumu zaidi kuliko tunavyoweza kuelewa. Kuna nafasi kwetu katika amri za Mungu kwa ajili yetu na ujuzi Wake wa kimbele jinsi tutakavyoitikia amri zake.

Yesu alifundisha, “Amin, nawaambia, kama mkiwa na imani wala msiwe na shaka… bali hata mkiuambia huu mlima, ‘Ngʼoka, ukatupwe baharini,’ litafanyika” (Mathayo 21:21). Imani ni muhimu sana katika kutembea kwetu na Mungu (Waebrania 11:6). Hata kiasi kidogo cha imani kinaweza kutimiza mambo makubwa-si kwa sababu imani ni nguvu maalum tuliyo nayo bali kwa sababu lengo la imani yetu, Mungu Mwenyewe, ndiye mwenye uwezo wote, na atuuliza tumwamini Yeye.

Imani pia ni muhimu katika wokovu, lakini hata ile imani inayotuokoa haibadilishi mpango wa Mungu. Mungu alituchagua katika Kristo kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu (Waefeso 1:4), na tunapewa imani kama karama (Waefeso 2:8-9). Baada ya wokovu, tunaendelea kutembea kwa imani (2 Wakorintho 5:7). Na kutembea huko kwa imani kunaendelea kukamilisha mpango wa Mungu: “Kwa maana sisi ni kazi ya mikono ya Mungu, tulioumbwa katika Kristo Yesu, ili tupate kutenda matendo mema, ambayo Mungu alitangulia kuyaandaa tupate kuishi katika hayo (Waefeso 2:10). Kuanzia mwanzo hadi mwisho, mpango wa Mungu unatimia, Anapotumia watu waliojazwa na Roho, waliojazwa na imani kuzaa matunda Yake ulimwenguni.

Waebrania 11 inajulikana kama sura ya imani. Kifungu hiki kinatoa mifano mingi ya wahusika wa kibiblia ambao waliishi kwa ajili ya Mungu kwa imani. Mwandishi wa Waebrania anasisitiza mifano yao kama mifano nzuri kwetu kufuata. Licha ya matatizo na magumu yao mengi, watu hawa walionyesha kwamba Mungu alikuwa akifanya kazi kupitia imani yao kwa njia ambazo zilibadilisha maisha yao wenyewe na historia. Andiko la Waebrania 11:30 laeleza kwa ufupi tukio moja katika maisha ya Yohsua: “Kwa imani kuta za Yeriko zilianguka, baada ya watu kuzizunguka kwa siku saba.” Je, imani ya Yoshua ilibadilisha mpango wa Mungu? Je, kuzunguka kwa majeshi hatimaye kulimshawishi Mungu kuchukua hatua katika siku ya saba? Au je, Mungu alipanga kuangusha kuta za Yeriko muda wote huo? Jibu la kibiblia ni kwamba ilikuwa mapenzi kuu ya Mungu kushinda Yeriko, na Alitumia mtu mwaminifu na watu watiifu kukamilisha mpango Wake.

Imani haibadilishi mpango mkuu wa Mungu, lakini ni sehemu muhimu ya maisha ya Kikristo (2 Wakorintho 4:18). Imani inajumuisha jinsi tunavyopata kumjua Mungu, jinsi tunavyoishi kwa ajili Yake, na jinsi tunavyomshirikisha na wengine.

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je, imani inaweza kubadilisha mpango wa Mungu?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries