settings icon
share icon
Swali

Je, maombi yanabadilisha fikra za Mungu?

Jibu


Swali hili linaweza kujibiwa vizuri kwa kugawanywa liwe maswali mawili: 1) Je, maombi yanabadilisha fikra za Mungu? na 2) Je, maombi yanabadilisha mambo? Jibu la kwanza ni, hapana, Mungu habadilishi fikra zake. Jibu la pili ni, ndio, maombi yanabadilisha mambo. Kwa hivyo, jinsi gani maombi yanaweza kubadilisha hali bila kubadilisha fikra za Mungu?

Kwanza kabisa, ili Mungu abadilishe fikra zake, angehitaji kuboresha nafsi yake kwa njia fulani. Kwa maneno mengine, ikiwa Mungu angebadili fikra zake, hatua hiyo ingeonyesha kuwa njia yake ya kwanza ya kufikiri ilikuwa duni,lakini, kwa sababu tuliomba, aliboresha mpango wake kuhusu hali yetu. Tunabadilisha fikra zetu tunapoona njia bora ya kufanya kitu. Tulifikiria A lakini tukagundua kuwa B ilikuwa bora, kwa hivyo tunabadilisha fikra zetu. Lakini, kwa kuwa Mungu anajua mambo yote, mwanzo kutoka mwisho ( Ufunuo 22:13; Waefeso 1:4), haiwezekani kwake kuboresha mpango wowote ambao amefanya. Mipango yake tayari ni kamili ( 2 Samweli 22:31), na amesema kuwa mipango yake itafanikiwa (Isaya 46:9-11).

Je, inawezekana kuwa na maandiko kama Kutoka 32:14 ambayo yanaonekana kuonyesha kuwa Mungu “alijuta” kuhusu hatua yake? Neno la kiebrania nacham mara nyingi linatafsiriwa kama “kujuta” au “ kubadilisha fikra,” linaweza pia kuwa na maana ya “huzuni” au “kuleta faraja.” Mwanzo 6:6 ni mara ya kwanza ya neno hili linapotumika kuhusiana na Bwana: “BWANA akaghairi kwa kuwa amefanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.” Hii inaonekana kumaanisha kwamba Mungu alikuwa na mawazo mengine kuhusu uamuzi wake wa kuumba binadamu.Lakini, kwa kuwa njia za Mungu ni kamili, tunahitaji kutafuta ufahamu mbadala. Ikiwa tunatumia ufafanuzi wa pili wa neno linalotafsiriwa “kujuta,” tunaweza kuelewa aya hii kuwa maovu ya mwanadamu ndiyo yalisababisha huzuni mkubwa katika moyo wa Mungu, hasa kwa kuangazia kile ambacho anapaswa kufanya ili kuwarejesha.

Yona 3:10 ni mfano mwingine wa neno la kiebrania nacham: “ Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda;asilitende.” Kwa maneno mengine, Mungu alipata faraja katika ukweli kwamba Hakuhitaji kuwaangamiza Wanineva kama vile Alivyosema Angefanya. Hakubadilisha fikra zake; kwa sababu alikuwa anajua watatubu.Matendo yake ni sehemu ya mpango wake mkubwa ulioundwa kabla Hajaumba ulimwengu. Yeremia 18:8 inasaidia kuelezea dhana hii: “ Ikiwa taifa lile nililolitaja litageuka, na kuacha maovu yake nitaghairi,nisitende mabaya yale niliyoazimia kuwatenda.”Mungu habadili fikra zake ; anapata faraja katika ukweli kwamba toba ya mwanadamu itapunguza matokeo ambayo yeye, katika haki yake, tayari amethibitisha.

Kwa hivyo, ikiwa maombi hayabadili fikra za Mungu, kwa nini tunaomba? Je, maombi yanabadilisha hali zetu? Ndio. Mungu hufurahi kubadili hali zetu kwa kujibu maombi yetu ya imani. Yesu alituagiza, “kusali siku zote na kutokataa tama” (Luka 18:1). 1 Yohana 5:14-15 pia hutukumbusha kwamba, tunapoomba kulingana na mapenzi ya Mungu, Yeye husikia na hujibu. Neno muhimu ni “kulingana na mapenzi yake.” Mapenzi hayo pia yanajumuisha wakati wake.

Tunaweza kuifikiria hivi: baba anapanga kumpa bintiye urithi muhimu anapofikisha umri wa miaka 16. Anajua akifika wakati huo atakuwa wa kutosha kwa jukumu la kuimiliki. Lakini pia anapanga kusubiri kumpa hadi wakati atakapoomba , kwa sababu anataka atambue thamani ya zawadi kama hiyo. Lakini akiwa na umri wa miaka 11, anaanza kuomba zawadi hiyo. Anaomba, anatathmini, na anakasirika alipofikisha miaka 12, 13, na 14 na bado hana urithi huo. Anakua mkubwa kidogo na anaacha kuomba, lakini kisha akiwa miaka 16 anamwendea baba yake kwa njia yenye busara, anaelezea haja yake ya urithi huo, na kuonyesha imani yake kwamba baba yake atatimiza haja hiyo. Kwa muda mfupi sana, baba yake kwa furaha anamkabidhi. Je, alibadili fikra yake? Hapana, alikuwa ameazimia kumpa. Je, alihitaji kuomba? Ndio, hiyo ilikuwa sehemu ya uamuzi wake.

Vivyo hivyo, Baba wetu wa mbinguni anatualika tumwombe kila tunachohitaji. Anafurahi kutupa ikiwa kitu hicho kipo ndani ya mpango wake. Anajua hatuelewi wakati wake kila mara, lakini anatarajia tutumaini na kutokuwa na shaka (Yakobo 1:5-6; Mathayo 6:8). Maombi yetu husaidia kuziunganisha mioyo yetu na moyo wake mpaka mapenzi yake yawe lengo letu kuu (Luka 22:42). Anaahidi kusikiliza na kutimiza tamaa za mioyo yetu wakati mioyo yetu ni yake (Zaburi 37:4; 2 Mambo ya Nyakati 16:9).

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je, maombi yanabadilisha fikra za Mungu?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries