settings icon
share icon
Swali

Je, inamaanisha nini kuwa huru kutoka kwa dhambi?

Jibu


Mithali 20:9 inauliza swali “Nimeuweka moyo wangu safi; mimi ni safi na sina dhambi?” sisi sote tunaweza kujitambulisha na hilo. Ikiwa sisi ni waaminifu kwa nafsi zetu, tunajua bado tunatenda dhambi. Kwa hivyo ni kwa nini Warumi 6:18 inasema, “Nanyi, mkiisha kuwekwa huru mbali na dhambi, mmekuwa watumwa wa haki?” Je, huu ni mkinzano?.

Dhambi inaweza kufafanuliwa kuwa “wazo lolote, au nia inayopungukiwa na utakatifu wa Mungu” (Warumi 3:23). Dhambi ina tabaka nyingi. Kuna matendo maalum au mawazo ambayo ni dhambi. Mauaji, uzinzi, na wizi ni dhambi (Kutoka 20:1-17). Hata tamaa ya kuua, uzinzi, na wizi ni dhambi (Mathayo 5:21, 28). Lakini dhambi ni zaidi ya hayo. Tunatenda dhambi kwa sababu sisi ni wenye dhambi. Kwa kuwa Adamu alitenda dhambi kwanza katika bustani mwa Edeni (Mwanzo 2:17; 3:17-19), kila mtu aliyezaliwa amerithi asili ya dhambi kutoka kwake (Zaburi 51:5; Warumi 3:23; 5:12). Hatuwezi kujizuia kutenda dhambi kwa sababu ni asili yetu kufanya hivyo. Si lazima ndege afunzwe jinsi ya kujenga kiota na kulalia mayai yake ili yawe joto. Ni asili yake kufanya hivyo. Si lazima mtoto afundishwe kuwa mbinafsi na mwenye kudai vitu vingi. Hiyo huja kwa kawaida.

Hata hivyo, hatukuumbwa kuwa wenye dhambi. Tuliumbwa na Mungu kwa mfano wake (Mwanzo 1:27). Ubinadamu ni kazi yake kuu (Waefeso 2:10; Zaburi 8:4-6). Tulikusudiwa kuishi katika ushirika na Muumba wetu. Lakini kwa sababu ya dhambi, hatuwezi kuingia katika uwepo wake (Habakuki 1:13). Yesu alipokufa msalabani, alijitwika dhambi zote za ulimwengu (2 Wakorintho 5:21; 1 Yohana 2:2). Kwa kuichukua adhabu ya dhambi zetu, alifuta deni ambalo kila mmoja wetu anadaiwa na Mungu (Wakolosai 2:14). Pia aligeuza laana ya asili yetu ya kale, ambayo inatufanya tuwe watumwa wa tamaa na nia za dhambi (Wagalatia 3:10,13). Kabla ya mtu kukutana na Yesu, yeye huwa mtuwa wa asili ya dhambi (Warumi 7:25; 2 Petro 2:19). Katika wakati wa kuokoka, tunapewa asili mpya ambayo imewekwa huru kutoka kwa dhambi (Warumi 6:18; 8:2). Sura nzima ya Warumi 6 anaeleza hili kwa kina. Mstari wa 14 unasema, “Kwa maana dhambi haitakuwa na mamlaka juu yenu, kwa sababu hampo chini ya sheria, bali chini ya neema.”

Kuwa huru kutoka dhambi inamaanisha kwamba wale ambao wamemfanya Yesu kuwa Bwana wa maisha yao si watumwa wa dhambi tena. Tuko na uwezo, kupitia kwa Roho Mtakatifu kuishi maisha ya ushindi juu ya dhambi (1 Wakorintho 15:56-67; Warumi 8:37). Kama vile tulivyofuata tamaa za mwili, wale walio “katika Kristo Yesu” sasa wanamfuata Roho Mtakatifu (Warumi 8:14; Wagalatia 5:24). Kwa sababu tunaisha katika ulimwengu ulioanguka na bado ni viumbe vya kimwili, bado tutatenda dhambi (1 Yohana 1:9; 2:1; Warumi 7:21-22). Lakini wale wanaomfuata Kristo hawafanyi dhambi kuwa chaguo la maisha (1 Yohana 2:1-6; 3:6-10; Warumi 6:2).

Wale ambao wamezaliwa mara ya pili (Yohana 3:3) wamepokea asili mpya. Ingawa utu wa kale ulituvuta katika kujiburudisha, asili mpya hutuvuta kwa utakatifu (2 Wakorintho 5:17). Kuwa huru kutoka kwa dhambi ina maana kwamba dhambi tena haina uwezo iliokuwa nayo hapo awali. Ngome ya ubinafsi, uchoyo, na tamaa imevunjwa. Uhuru kutoka kwa dhambi huturuhusu kujitoa wenyewe kama watumwa wa hiari wa Bwana Yesu Kristo, ambaye anaendelea kufanya kazi ndani yetu ili kutufanya tufanane naye zaidi (Warumi 6:18; 8:29; Wafilipi 2:13).

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Je, inamaanisha nini kuwa huru kutoka kwa dhambi?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries