settings icon
share icon
Swali

Ni kwa nini tunaomba kabla ya kula chakula?

Jibu


Wakristo mara nyingi huomba kabla ya chakula, wakitoa shukrani kwa Mungu kwa chakula wanachokaribia kula. Maombi ya kabla ya chakula yanaweza kuwa rahisi “asante” kwa Mungu kwa chakula au maombi marefu zaidi ya shukrani kwa ajili ya maandalizi yake yote maishani mwetu. Katika kusali kabla ya vyakula, tunafuata kielelezo cha Bwana Yesu, ambaye maombi yake mara nyingi ni kielelezo chetu.

Katika matukio mawili ambapo Yesu alilisha kimuujiza umati wa watu kwa mikate michache na samaki, Yeye “alitoa shukrani” (Mathayo 14:19-21; 15:34-36). Katika tukio la kwanza, Aliwalisha wanaume 5,000, pamoja na wanawake na watoto, kwa mikate mitano na samaki wawili. Katika tukio la pili, Aliwalisha zaidi ya watu 4,000 kwa mikate saba na samaki wachache. Katika Mlo wa Jioni wa Mwisho, Yesu aliweka tena mfano wa kutoa shukrani. Alipowakabidhi wanafunzi wake kikombe na mkate, akawaambia wale na kunywa vitu hivyo ambavyo vilikuwa ishara ya mwili na damu yake, Alishukuru. Alipowatokea wale watu wawili njiani kuelekea Emau baada ya kufufuka Kwake, Alisimama kwa muda ili kula nao, na “akachukua mkate, akashukuru, akaumega, akaanza kuwagawia” (Luka 24:30).

Mtume Paulo aliendelea na mfano huu wa kusali kabla ya kula, kama ilivyoandikwa katika Matendo 27. Katika kisa hiki, Paulo alikuwa kwenye meli pamoja na watu wengine 276 wakati tufani ilipoipiga meli. Baada ya siku kumi na nne za kutokula, Paulo aliwahimiza mabaharia na abiria wengine wale chakula ili kuishi. “akachukua mkate, akamshukuru Mungu mbele yao wote, akaumega akaanza kula” (Matendo 27:35). Hata licha ya hatari na mazingira ya kutisha, Paulo alitulia ili kumshukuru Mungu kabla ya chakula.

Tunapomshukuru Mungu kwa kutupa mkate wetu wa kila siku, tunakiri kwamba vitu vyote hutoka kwake (Waefeso 5:20; Warumi 11:36). Yeye ndiye chanzo cha kila kitu tulicho nacho, na kusali kabla ya kula kama mazoea hutukumbusha ukweli huo. Kuomba kabla ya kula kwa moyo wa shukrani huleta utukufu kwa Mungu na kuelekeza akili zetu kwenye upendo Wake mkuu kwa watoto Wake na baraka anazowapa wale walio Wake.

English



Rudi kwa ukurasa wa nyumbani wa Kiswahili

Ni kwa nini tunaomba kabla ya kula chakula?
Shiriki ukurasa huu: Facebook icon Twitter icon Pinterest icon Email icon
© Copyright Got Questions Ministries